KKKT lakemea mavazi ya kubana
Wakati huo huo, usharika wa Tabata Kuu umemuomba mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dk Alex Malasusa kutoa tamko la wazi kupinga uamuzi wa kanisa hilo nchini Marekani na Ulaya kuruhusu ndoa za mashoga.
Ombi hilo lilitolewa mwishoni mwa wiki na Mchungaji Erasto Ailla wa usharika huo wa KKKT alipohubiri kwenye maadhimisho ya siku kuu ya Krismasi ya kuadhimisha miaka 2009 ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo. Mchungaji huyo pia aliongoza sala maalum ya kupinga vitendo hivyo.
Mchungaji Ailla, akionyesha kusikitishwa na vitendo hivyo kwa makanisa ya nchi za Magharibi, alisema taarifa za kanisa hilo nchini Marekani na barani Ulaya kubariki ndoa za mashoga na wengine kuongoza ni kumkejeli Mungu ambaye ametamka wazi kwamba waovu wa aina hiyo hawatauona ufalme wa Mungu.
Alimuomba Dk Malasusa tamko la kupinga uamuzi huo kwa Tanzania na Afrika kwa ujumla na kwamba yeye anaamini kwamba kanisa hilo barani Afrika halitakubali kuruhusu mashoga kuoana kwani ni kinyume na maagizo ya Mungu.
"Kwa kuanzia, nawaomba waumini wote usharika huu tuwe wa kwanza kupinga na sasa tusimame, tufumbe macho na kuomba sala maalum ya kukataa ushoga ndani ya kanisa na kukiri wazi kwamba mashoga... wanamchukiza Mungu kama wale wa Sodoma na Gomola," alisisitiza na kuwaongoza waumini kwa sala maalumu ambayo pamoja na mambo mengine pia ilikuwa inakataa ushoga kwa mbinu zote.
Kanisa la Kilutheri nchini Marekani liliruhusu ndoa za mashoga baada ya uamuzi huo kupitishwa kwenye mkutano wake mkuu, na kuwa kanisa la pili baada ya Anglican ambalo pia ni la Marekani.

